UHABA WA MADARASA TATIZO WANAFUNZI 1266 WAKOSA MASOMO



Wanafunzi 1266 waliochaguliwa kujiunga kidato cha kwanza 2018/2019 mkoani Lindi wameshindwa kujiunga na kuanza masomo kutokana na ukosefu wa vyumba vya madarasa.
Hayo yalibainishwa jana na katibu tawala(RAS) wa  mkoa wa Lindi, Rehema Madenge alipozungumza kwenye kikao cha kamati ya ushauri ya mkoa(RCC) kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi ya mkuu wa mkoa,iliyopo katika manispaa ya Lindi.
Madenge alisema katika zoezi la uchaguzi wa wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2019, wanafunzi 11808 walichaguliwa na kupangiwa shule watakazo jiunganazo kwa ajili ya masomo.Ambapo kati ya wanafunzi hao waliochaguliwa ni wasichana 6124 na wavulana 5684.
Alisema kati ya wanafunzi hao waliochaguliwa,bado wanafunzi 1266 hawajajiunga kwenye shule walizopangiwa kutokana na kukosekana kwa vyumba vya madarasa.Huku akibainisha kwamba wanafunzi hao ni wasichana 602 na wavulana 664.

Madenge alizitaja halmashauri ambazo baadhi ya wanafunzi waliochaguliwa wameshindwa kuanza masomo kutokana na tatizo hilo kuwa ni,majina na idadi ya wanafunzi kwenye mabano ni Kilwa(434),Lindi(443),Nachingwea(127) na Ruangwa wanafunzi 262.

Katibu tawala huyo wa mkoa wa Lindi alisema kushindwa kujiunga kwa wanafunzi hao mapema kumesababishwa na upungufu wa vyumba vya madarasa 39 ambavyo vingeweza kukidhi mahitaji.

"Wilaya inayoongoza kwakuwa na upungufu wa vyumba vya madarasa ni Kilwa ambayo inaupungufu wa vyumba kumi nanne hadi sasa.Ruangwa vyumba kumi na moja,Lindi vyumba kumi na wilaya ya Nachingwea ni vyumba vinne,"alisema Madenge.

Alisema kufuatia hali hiyo,mkuu wa mkoa wa Lindi,Godfrey Zambi ameziagiza halmashauri ambazo wanafunzi waliochaguliwa wameshindwa kuanza masomo zikamilishe ujenzi wa vyumba vya madarasa.Ambapo amezitaka ifikapo tarehe 15,mwezi Februari,mwaka huu ziwe zimekamilisha ujenzi huo.

Kufuatia hali hiyo baadhi ya wadau wa elimu mkoani humu walitoa maoni yao yanini kifanyike.Miongoni mwa wadau hao ni Mohammed Mussa anaeishi katika manispaa ya Lindi.Ambae alisema wazazi na walezi hawanabudi kuungana ili kutatua changamoto zilizopo kwenye sekta ya elimu.Badala ya jukumu hilo kuachiwa serikali peke yake.

Mohammed alisema alitoa ushauri huo wa jumla kutokana na mkoa wa Lindi kuendelea kupata matokeo mabovu ya kiwanga cha ufaulu.Ambao matokeo ya mtihani wa kidato cha pili umeshika nafasi ya 24 kati ya 26 iliyopo Tanzania bara.

No comments: