Kampuni ya Ufaransa yaondoa maboksi milioni 12 ya maziwa sokoni



Ilani ya kuwatadharisha walaji bidhaa ya maziwa ya watoto iliyoondolewa sokoni.
Zaidi ya maboksi milioni 12 ya maziwa ya watoto yanayotengenezwa na kampuni ya maziwa Lactalis ya Ufaransa yameondolewa madukani kutoka nchi 83 kwa hofu ya kuwa yamechafuliwa na vijidudu aina ya salmonella vinayosababisha sumu katika chakula.
Mkuu wa kampuni hiyo ya maziwa nchini Ufaransa Jumapili amethibitisha kuwa bidhaa zake zinarudishwa kiwandani kutoka nchi zote Ulaya, Afrika na Amerika ya Kusini na Asia baada ya Salmonella ilipogunduliwa katika moja ya mitambo yake mwezi wa Disemba 2017. Lakini Marekani, Uingereza na Australia hazikuathirika na tatizo hilo.
Maafisa wa kampuni hiyo wamesema kuwa wanaamini kuwa kuathiriwa kwa bidhaa zao na sumu hiyo kumetokana na matengenezo yaliofanyika katika kiwanda chao cha Celia huko Craon, kaskazini magharibi ya Ufaransa.
Emmanuel Besnier ameliambia gazeti la kila wiki Le Journal du Dimanche kuwa kampuni hiyo ya familia yake, ambayo ni moja ya kiwanda cha maziwa kikubwa kuliko vyote duniani, italipa fidia kwa “kila familia ambayo iliathiriwa na hali hiyo.”
Gazeti hilo limesema kuwa watoto 35 walionekana kuwa na vijidudu hivyo nchini Ufaransa, mmoja nchini Spain na pia kunauwezekano yuko mwengine Ugiriki.

Kwa mujibu wa wataalamu wa afya Salmonella inaweza kusababisha kuharisha kulikopindukia, maumivu ya tumbo, kutapika na kupungukiwa kwa maji mwilini kwa kiwango kikubwa. Pia inaweza kuhatarisha maisha ya mwanadamu, hususan watoto wadogo.
Waziri wa Kilimo wa Ufaransa amesema kuwa bidhaa kutoka katika kiwanda hicho zitaendelea kupigwa marufuku wakati uchunguzi unaendelea.

No comments: