Baadhi ya polisi wakiwa katika eneo la tukio Ukonga Mazizini wakidumisha ulinzi ili wananchi wasiendelee kuleta vurugu katika eneo hilo.


Kufuatia sintofahamu iliyokuwa inaendelea maeneo ya Mombasa Gongo la Mboto kati ya wananchi na jeshi la polisi na kupelekea baadhi ya raia kujeruhiwa na polisi kwa kile kinachodaiwa kuwa polisi walikuwa wanalipiza kisasi kufuatia kuuawa kwa askari mmoja wa kikosi cha 'Field Force Unit' (FFU)
Mkuu wa Wilaya ya Ilala Sophia Mjema ametembelea eneo hilo na kusikitishwa na kitendo cha jeshi la polisi kuchukua sheria mkononi na kujeruhi watu ambapo ameagiza wote waliohusika kufanya matukio hayo kuchukuliwa hatua za kisheria.

"Nimeambatana na RPC Salum Hamduni hivyo kwa wale walihusika hatua zitachukuliwa, na wale waliojeruhiwa watatibiwa, pia tumewachukua baadhi ya wananchi ambao wamehaidi kutoa ushirikiano hivyo  tutalifanyia uchunguzi na kutenda haki" Alisema DC Mjema.
Mkuu wa wilaya ya Ilala bi. Sophia Mjema akiongea na wananchi wa eneo la Ukonga Mazizini na kusikiliza kero zao baada ya kudai kupigwa na kupokonywa mali zao na watu wanaodhaniwa kuwa ni askari wa FFU.
DC Mjema amewataka wananchi wote walioharibiwa mali zao wajiorodheshe na serikali ya wilaya italifanyia kazi, huku akisisitiza hakukuwa na sababu ya kuchukua sheria mkononi wakati kulikuwa na mbadala wa kulichunguza suala hilo na kulipatia utatuzi.

Mkuu huyo wa wilaya ya ilala amewaomba wananchi watulie na waendelee na shughuli zao kwani hilo siyo jambo kubwa la kupelekea watu wauane na wavuruge amani ya nchi.

Sintofamhamu hiyo imedumu kwa siku tatu kufuatia kifo cha askari wa kikosi cha FFU ambapo inadaiwa aliuawa na wananchi jambo lililopelekea vurugu hizo, baina ya jeshi la polisi na wananchi.



No comments: